Uharamu Wa Kunyoa Ndevu

 

Uharamu Wa Kunyoa Ndevu

 

Alhidaaya.com

 

 

Hakika zilikuja Hadiyth nyingi zinazoamrisha kufuga ndevu kama kauli ya Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa sallam) aliosema:

قوله صلى الله عليه وسلم: أحفوا الشوارب وأعفوا اللحى. رواه الترمذي وقال: حديث صحيح

Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) amesema:

 

"Punguzeni masharubu na fugeni ndevu". 

 

وقوله صلى الله عليه وسلم: جزوا الشوارب وأرخوا اللحى، خالفوا المجوس. رواه مسلم

Na kauli ya Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa sallam) aliyosema:

 

"Kateni masharubu, ziwekeni kwa wingi ndevu, wapingeni Majuusi".

 

 

وقوله صلى الله عليه وسلم: أعفوا. بفتح الهمزة: أي اتركوها بحالها لتكثر وتغزر؛ لأن في ذلك جمالاً للوجه وزينة للرجل، وهذا أمر صريح يفيد الوجوب كما هو مقرر في الأصول، ونص العلماء على تحريم حلقها، قال شيخ الإسلام ابن تيمية: ويحرم حلق اللحية

Na kauli ya Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa sallam) "fugeni",

Yaani ziacheni ziwe nyingi kwa sababu ndevu ndio uzuri wa mwanaume na hii amri ni ya uwajibu kama wanavyosema ‘Ulamaa wa Uswuwlul Fiqh.

 

قال ابنُ عَبْدِ البَرِّ - رحمه الله تعالى

(ويحرم حلق اللحية ، ولا يفعله إلا المخنثون من الرجال) [التمهيد[

Amesema Ibn ‘Abdil-Barri (Allaah Amrehemu):

 

“Na ni haramu kunyoa ndevu, na hawanyoi isipokuwa Makhanithi katika wanaume”.

 

Khanithi ni nani?

 

Ni yule mwenye tabia za kike, anapenda mambo ya kike kike.

 

قال الشنقيطي (أضواء البيان)، أعظم الفوارق الظاهرة بين الرجل والمرأة هي االحية

Amesema Al-Imaam Ash-Shanqiitwiy (Allaah Amrehemu):

 

"Vitofautisho vilivyo wazi mno baina ya mwanamme na mwanamke ni ndevu".

 

قال ابن القيم (التبيان)، واما شعر اللحية ففيه منافع، منها : الزينة، والوقار مايرى على ذوي اللحى، ومنها، التمييز بين الرجال والنساء...

Amesema Ibn Al-Qayyim (Allaah Amrehemu):

"Na ama ndevu, basi ndani yake kuna manufaa (mengi), miongoni mwa hayo ni pambo na upole unao onekana kwa wafuga ndevu, pia (katika faida zake) ni kupambanua baina ya wanaume na wanawake".

 

Wanachuoni wengine wanasema:

 

"Kunyoa ndevu (jambo hilo) huzingatiwa kuwa ni kujifananisha na wanawake".

 

Wanachuoni ni wengi sana waliozungumzia kuhusu uharamu wa kunyoa ndevu.

 

Kasema Ibn Taymiyyah (Allaah Amrehemu):

 

((Ni haramu kunyoa ndevu)).

 

وقال ابن عابدين في رد المحتار: ويحرم على الرجل قطع لحيته

Na kasema Ibn ‘Aabidiyn (Allaah Amrehemu):

 

((Na ni haramu kwa mwanaume kukata nywele zake za ndevu)).

 

وقال العدوي في الحاشية على شرح رسالة أبي زيد: يحرم إزالة شعر اللحية

Na kasema Al-‘Adawiy (Allaah Amrehemu):

 

((Ni haramu kuondoa nywele za ndevu)).

 

 

Baadhi ya Fataawa kuhusu uwajibu wan ufuga ndevu na uharamu wa kuzinyoa, kutoka kwa Wanachuoni wakubwa wa kutegemewa:

 

 

Hukumu Ya Kunyoa Au Kupunguza Ndevu Na Isbaal

 

Swali

Naomba muelekezo katika haki kwa kuwa nimechanganyikiwa, kuhusiana na suala la kunyoa ndevu na Isbaal? Ipi hukumu ya kunyoa ndevu

 

Jibu:

kuzinyoa ni Haramu, na kuzifupisha ni Haramu. Na Sunnah ni kuziacha ndevu kama zilivyo kwa maadhimisho ya uongofu wa Mtume Muhammad (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam). Usimjali yeyote anayesema kuwa kufupisha inajuzu au wanaojaribu kushawishi kukata ndevu kwa njia yoyote kuwa inajuzu, hata akikwambia kuwa ni mtu mwenye elimu, na yeye kusema kweli ni mtu asiyekuwa na elimu. Sunnah inamgusa kila mtu.

 

Na Isbaal ya vazi (kuvaa nuo ikavuka mafundo ya miguu) ni Haramu.

 

"Chenye kuvuka chini ya mafundo ya miguu katika vazi hupelekea motoni” [Al-Bukhaariy]

"Atayeteremsha vazi lake kwa kiburi, Allaah hatomtazama siku ya Qiyaamah." [Tirmidhiy]

 

“Watu watatu Hatowasemesha Allaah siku ya Qiyaamah, na Hatowatazama, na Hatowatakasa, na watapata adhabu iumizayo; (Hao ni) al Musbil – Mwenye kuburuza nguo yake, mwenye kutoa na kukizungumzia alichokitoa, Na mwenye kuuza bidhaa zake kwa kutumia kiapo cha uongo” [Muslim]

 

´Allaamah ´Abdul-´Aziyz bin ´Abdillaah Aal ash-Shaykh

 

 

Mwenye Kunyoa Ndevu Anapata Madhambi

 

Swali:

Mwenye kunyoa ndevu zake anapata madhambi kwa kuzinyoa?

 

Jibu:

Ndio, anapata madhambi. Kwa kuwa kufuga ndevu ni wajibu na kuzinyoa ni haramu. Dalili ya hilo, imekuja katika Sunnah kutoka kwa Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) katika Hadiyth nyingi anaamrisha ndani yake Nabiy (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) kufuga ndevu, kuzirefusha, kuziachia na kuziacha kwa wingi. Matamshi yote haya yamekuja kutoka kwa Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam). Na imekuja vilevile jitofautisheni na washirikina na jitofautisheni na majusi. Na imekuja vilevile:

 

"Allaah Kawalaani wanaume wanaojifananisha na wanawake. Na wanawake wanaojifananisha na wanaume."

 

Na ni jambo linalojulikana kule mwanaume kunyoa ndevu zake, anakuwa amejifananisha na wanawake ambao Allaah Kawaumba bila ya ndevu usoni. Mwenye kufanya hivyo atakuwa anapata madhambi na katumbukia katika maasi, kwa kwenda kwake kinyume na maamrisho na kujifananisha kwake na wanawake.

 

´Allaamah ´Abdul-Muhsin bin Hamad al-´Abbaad

http://www.alharamain.gov.sa/index.cfm?do=cms.scholarallsubjects&schid=9636

 

 

Kunyoa Ndevu Ni Kujifananisha Na Wanawake Na Ni Laana

 

Haijuzu kwa mwanaume kujifananisha na wanawake katika mavazi yao, kutembea kwao, kuongea kwao, kujipendezesha kwao wanawake. Haijuzu kwake hilo kwa kuwa yeye ni mwanamume. Yahitajika kwake nguvu na ukakamavu, hakuhitajiki kwake ulaini na kujiachia achia hivi ilihali ni mwanaume. Asifike kwa sifa za wanaume.
Kadhalika katika kujifananisha na wanawake ni kunyoa ndevu, hii ni aina kubwa katika aina za kujifananisha na wanawake, kunyoa ndevu akawa mwanaume kama mwanamke...

Kitu kinachomtofautisha mwanaume na mwanamke ni ndevu, hivyo [mwanaume] akinyoa ndevu zake huwezi kutofautisha kati ya uso wa mwanamke na uso wa mwanamume. Inatoweka alama inayowapambanua. Huku ni kujifananisha wanaume kwa wanawake.

Allaah Kamuumba nazo mwanaume na kumnyima nazo mwanamke. Hivyo kamlaani Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) anaelifanya, na laana ni dalili ya kuonesha kuwa ni dhambi kubwa katika madhambi makubwa. Ni wajibu kwa wanaume kujitofautisha na wanawake, na ni wajibu kwa wanawake kujitofautisha na wanaume. Huu ndo wajibu.

 

وَلَيْسَ الذَّكَرُ كَالْأُنثَىٰ

Na mwanamme si kama mwanamke. [Aal-´Imraan: 36]

 

Ama akiwa mwanamume kama mwanamke au mwanamke kama mwanamume, hali itabadilika - Laa Hawla walaa Quwwata illa biLlaah. Na yeye kajifananisha na sifa ya wanawake.

Lakini ukimwambia wewe ni kama mwanamke atakukasirikia au anaweza hata kukuua, ukimwambia [mnyoa ndevu] wewe ni kama mwanamke, atakuua au atakupiga. Ilihali yeye mwenyewe ndo anafanya jambo hili, anakuwa kama mwanamke.

 

Imaam Swaalih bin Fawzaan al-Fawzaan

 

 

Kufuga Ndevu Ni Sunnah Au Waajib?

 

Swali:

Ni ipi kauli sahihi kuhusu ndevu. Je ni Sunnah au wajibu?

 

Jibu:

Ni wajibu. Na dalili ya uwajibu wake ziko nyingi. Nabiy (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) kasema:

"Zirefusheni ndevu na mziache ziwe nyingi."

Kuna ibara mbalimbali ambazo ni nyingi zimethibiti kutoka kwa Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam). Na amesema:

"Wakhalifuni majusi, wakhalifuni washirikina."

Hizi ni dalili. Dalili zingine:

"Allaah Kamlaanii mwanaume mwenye kujifananisha na wanawake. Na mwanamke mwenye kujifananisha na wanaume."

Na mwanaume akinyoa ndevu zake anafanana na mwanamke. Mwanamke ndiye asiyekuwa na ndevu. Mwanaume akinyoa ndevu zake anakuwa kama mwanamke.

´Allaamah ´Abdul-Muhsin bin Hamad al-´Abbaad

http://www.alharamain.gov.sa/index.cfm?do=cms.scholarallsubjects&schid=9636

 

 

Ndevu Za Rusuli

 

Al-Bayhaqiy kapokea kwenye "Dalaail-un-Nubuwwah" kutoka kwa Hishaam bin al-'Aas al-Umawiy ambaye amesema:

"Mimi na mtu mwingine tulitumwa kwa mfalme wa Roma Heraclius kumlingania katika Uislamu..."

Baada ya hapo akahadithia tukio lirefu ambapo Heraclius alionesha picha za Rusuli. Rusuli walionekana kwa njia ifuatayo:

Nuwh ('Alayhis-Salaam) alikuwa na ndevu nzuri.

Ibraahiym ('Alayhis-Salaam) alikuwa na ndevu nyeupe.

Ya´quub ('Alayhis-Salaam) zilikuwa zinafanana na ndevu za baba yake Ishaaq.

'Iysaa ('Alayhis-Salaam) alikuwa na ndevu nyeusi sana.

Ibn Kathiyr kasema:

"Mnyororo wake (wa mapokezi) ni mzuri."

Abu Nu'aym al-Asbahaaniy kapokea katika kitabu chake "Dalaail-un-Nubuwwah" kupitia njia nyingine ya kwamba Muwsa ('alayhis-Salaam) alikuwa na ndevu zenye kujaa na Haaruun ('alayhis-Salaam) alikuwa anafanana na Muusa.

 

´Allaamah Hamuud bin ´Abdillaah at-Tuwayjiriy. Ar-Radd ´alaa man ajaaza Tahdhib-al-Lihyah, uk. 7

 

 

Nani Kasema Mnyoa Ndevu Hawezi Kuingia Motoni?

 

Swali:

Nimejadiliana mimi na ndugu zangu kuhusu ndevu. Wakaniingiza ndani ya utata na kunambia kuwa ndevu sio faradhi wala wajibu. Lau ingelikuwa ni wajibu kwa mfano mwenye kufanya hivyo angelikuwa anaingia Motoni pamoja na kuwa ananyoa ndevu zake.

 

Jibu:

Ni kipi kinachompa matumaini ya kutoingia Motoni? Mtenda madhambi anaingia Motoni. Huyu anasema kwamba anayenyoa ndevu zake hawezi kuingia Motoni? Ni mwenye kutishiwa na kukhofiwa kuingia Motoni na kupewa adhabu na tunajikinga kwa Allaah. Kila mwenye kuasi basi ni mwenye kukhofiwa juu yake adhabu. Ni nani aliyemwambia kwamba mwenye kunyoa ndevu hawezi kuingia Motoni?

Imaam Swaalih bin Fawzaan al-Fawzaan

http://www.alfawzan.af.org.sa/node/13054

 

 

Madai Kuwa ”Kufuga Ndevu Hakutowatoa Mayahudi Palestina”

 

Swali:

Tunapowakumbusha baadhi ya watu uharamu wa kunyoa ndevu wanatolea dalili Fataawa za wanachuoni wa kwenye Televisheni na kwamba imependekezwa. Halafu wanasema ya kuwa, mambo haya hayatowatoa Mayahudi Palestina.

 

Jibu:

Mfano wa maneno kama haya, bila ya shaka ni maneno ambayo ndani yake kuna kuchukulia usahali mambo ya Dini. Kufuga ndevu, hili ndio limekuja katika Sunnah kutoka kwa Nabiy wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) kwa kauli yake, kitendo chake na kukubali kwake hilo kwa hali ya kulinyamazia.

 

Nabiy (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) alikuwa ni mtu wa ndevu nyingi. Na Swahaba wake (Radhwiya Allaahu ´anhum) walitolea dalili ya kusoma kwake katika Swalaah zake za siri kwa kutikisika ndevu zake, yaani walijua ya kwamba huwa anasoma kwa kutikisika ndevu zake kando. Hivyo, alikuwa ni mtu wa ndevu nyingi (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam). Na Swahaba wake walikuwa ni watu wa ndevu. Na alikuwa anawaona na akalikubali hilo.

Na kumekuja kutoka kwake maamrisho ya kufuga ndevu. Akasema:

"Zirefusheni."

"Fugeni (ndevu) kwa wingi."

Kumekuja matamshi mengi kutoka kwa Nabiy (´Alayhis-Salaam). Hii ni amri ya wajibu na wala haisemwi kwamba ni katika mambo yanayopendekezwa.

 

Isitoshe katika kunyoa ndevu kuna kujifananisha na wanawake. Na Nabiy (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) anasema:

"Allaah Amlaani mwanaume anayejifananisha na wanawake. Na mwanamke anayejifananisha na wanaume."

 

Kule mtu kunyoa ndevu zake ni kujifananisha na wanawake. Anakuwa hana ndevu. Uso wake unakuwa kama uso wa mwanamke. Anakuwa amejifananisha nae. Yote haya ni katika dalili zinazoonesha uharamu wake.

 

Ama kutoka Mayahudi Palestina, hili linakuwa kwa nguvu za Waislamu na nguvu ya Imani yao. Na linakuwa vilevile kwa kushikamana kwao na Shari´ah na kusimama na yale yaliyo ya wajibu kwao. Wanakuwa na uwezo wa kimali na uwezo wa kimaana. Ni jambo linalojulikana ya kwamba, nguvu za kimali zinafaa ikiwa nguvu za kimaana zipo tayari; (na nguvu hizo za kimaana) ni kushikamana na amri za Allaah.

 

´Allaamah ´Abdul-Muhsin bin Hamad al-´Abbaad

http://www.alharamain.gov.sa/index.cfm?do=cms.scholarallsubjects&schid=9636

 

 

 

Kunyoa Ndevu Kwa Hoja Ya Kwamba Makafiri Na Wao Wanafuga Ndevu

 

Swali:

Baadhi ya watu wanasema mayahudi au baadhi ya washirikiana wanafuga ndevu zao hivi sasa na sisi tumeamrishwa kwenda kinyume nao...

 

Jibu:

Hatukuamrishwa kwenda kinyume nao katika kufuga ndevu. Tumeamrishwa kwenda kinyume nao katika kunyoa. Ama wakiachia ndevu zao basi wameafikiana na sisi. Kafiri ambaye amefuga ndevu zake ana sura bora kuliko kafiri ambaye ananyoa ndevu zake.

Imaam Swaalih bin Fawzaan al-Fawzaan

http://www.alfawzan.af.org.sa/node/5570

 

 

Yupi Imaam Bora, Haafidhw Mnyoa Ndevu Au Asiyenyoa Ndevu?

 

Swali:

Kuna Msikiti ambapo hakuna Imaam rasmi, lakini kuna ndugu wawili wazuri. Mmoja wao amehifadhi Msahafu mzima lakini anafupisha ndevu zake na anaswali huku amevaa suruwali, na mwengine amehifadhi sehemu kubwa ya Qur-aan na ameacha ndevu zake na anavaa mavazi ya kawaida. Yupi katika hawa wawili atangulizwe kuwa Imamu?

 

Jibu:

Atangulizwe yule ambaye kaacha ndevu zake na anavaa mavazi ambayo ni maarufu wanayovaa watu wa mji. Huyu ndiye atangulizwe kwa kuwa ni borakuliko huyo wa kwanza.

 

´Allaamah Swaalih bin Fawzaan

http://www.alfawzan.af.org.sa/alldroos?tid_1=160

 

Na Allaah Anajua zaidi

 

 

 

 

Share