Kisa Cha Nabiy Swaalih (عليه السلام) - 3

 

 

Kisa Cha Nabiy Swaalih ('alayhis-salaam)

 

Sehemu Ya 3

 

Alhidaaya.com

 

 

 

Njama Za Kumuua Nabiy Swaalih ('alayhis-salaam):

 

 

Baada ya kumuua ngamia, na kuendelea kumkanusha Nabiy Swaalih ('alayhis-salaam) na kukanusha risala aliyotumwa na Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa), wakapanga njama kumuua Nabiy Swaalih ('alayhis-salaam). Njama zao zimetajwa katika Aayah zifuatazo:

 

Maelezo zaidi ya kisa hiki katika kauli za Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) zifuatazo:

 

وَلَقَدْ أَرْسَلْنَا إِلَىٰ ثَمُودَ أَخَاهُمْ صَالِحًا أَنِ اعْبُدُوا اللَّـهَ فَإِذَا هُمْ فَرِيقَانِ يَخْتَصِمُونَ ﴿٤٥﴾

Na kwa yakini Tuliwapelekea kina Thamuwd ndugu yao Swaalih kwamba: Mwabuduni Allaah. Tahamaki wakawa makundi mawili yanayokhasimiana.

 

قَالَ يَا قَوْمِ لِمَ تَسْتَعْجِلُونَ بِالسَّيِّئَةِ قَبْلَ الْحَسَنَةِ ۖ لَوْلَا تَسْتَغْفِرُونَ اللَّـهَ لَعَلَّكُمْ تُرْحَمُونَ ﴿٤٦﴾

 (Swaalih) Akasema: Enyi kaumu yangu! Kwa nini mnahimiza uovu kabla ya mema; kwa nini msimwombe Allaah maghfirah ili huenda mkarehemewa?

 

قَالُوا اطَّيَّرْنَا بِكَ وَبِمَن مَّعَكَ ۚ قَالَ طَائِرُكُمْ عِندَ اللَّـهِ ۖ بَلْ أَنتُمْ قَوْمٌ تُفْتَنُونَ ﴿٤٧﴾

Wakasema: Tumepata nuksi kwa sababu yako na kwa wale walio pamoja nawe. (Swaalih) Akasema: Nuksi yenu iko kwa Allaah. Bali nyinyi ni watu mliojaribiwa.

 

وَكَانَ فِي الْمَدِينَةِ تِسْعَةُ رَهْطٍ يُفْسِدُونَ فِي الْأَرْضِ وَلَا يُصْلِحُونَ ﴿٤٨﴾

Na kulikuweko katika mji ule watu tisa wakifanya ufisadi katika ardhi na wala hawatengenei.

 

قَالُوا تَقَاسَمُوا بِاللَّـهِ لَنُبَيِّتَنَّهُ وَأَهْلَهُ ثُمَّ لَنَقُولَنَّ لِوَلِيِّهِ مَا شَهِدْنَا مَهْلِكَ أَهْلِهِ وَإِنَّا لَصَادِقُونَ ﴿٤٩﴾

Wakasema: Apishaneni kwa Jina la Allaah kwamba tutamhujumu (Swaalih) kwa siri usiku na ahli yake, kisha tutasema kwa jamaa yake wa karibu: Hatukushuhudia maangamizi ya ahli yake; nasi hakika ni wa kweli.

 

وَمَكَرُوا مَكْرًا وَمَكَرْنَا مَكْرًا وَهُمْ لَا يَشْعُرُونَ ﴿٥٠﴾

Wakapanga njama Nasi Tukapanga mipango ya kuvurumisha njama nao huku hawatambui.

 

فَانظُرْ كَيْفَ كَانَ عَاقِبَةُ مَكْرِهِمْ أَنَّا دَمَّرْنَاهُمْ وَقَوْمَهُمْ أَجْمَعِينَ ﴿٥١﴾

Basi tazama vipi ilikuwa hatima ya njama zao, kwamba Tuliwadamirisha na watu wao wote.

 

فَتِلْكَ بُيُوتُهُمْ خَاوِيَةً بِمَا ظَلَمُوا ۗ إِنَّ فِي ذَٰلِكَ لَآيَةً لِّقَوْمٍ يَعْلَمُونَ ﴿٥٢﴾

Basi hizo ni nyumba ni magofu kwa sababu ya yale waliyodhulumu. Hakika katika hayo kuna Aayah (ishara, zingatio, funzo n.k.) kwa watu wanaojua. [an-Naml: 45-52]

 

Kuhusu Kauli ya Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa):

 

 وَكَانَ فِي الْمَدِينَةِ تِسْعَةُ رَهْطٍ يُفْسِدُونَ فِي الْأَرْضِ وَلَا يُصْلِحُونَ ﴿٤٨﴾

Na kulikuweko katika mji ule watu tisa wakifanya ufisadi katika ardhi na wala hawatengenei.

 

Ina maana walikuwa wakilazimishia watu wa Thamuwd wakubaliane na rai zao   pamoja na njama zao kwa sababu wao walikuwa ni viongozi na vigogo wao. 

 

Al-Awfi kasema kwamba Ibn 'Abbaas (Radhwiya Allaahu ‘anhumaa) amesema: “Hawa ni watu waliomuuwa ngamia." [At-Twabariy 19:477]

 

 

Wakapanga njama kumuua Nabiy Swaalih (‘alayhis-salaam) pindi atakapolala  usiku akiwa pamoja na aila yake,  wamuue  kisha wawaambie jamaa zake Nabiy Swaalih ('alayhis-salaam) kuwa  wao hawajui lolote kuhusu yaliyotokea usiku huo na kwamba wao wanasema kweli kwa sababu hakuna wala mmoja wao aliyeshuhudia jambo. Kauli ya Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa):

 

قَالُوا تَقَاسَمُوا بِاللَّـهِ لَنُبَيِّتَنَّهُ وَأَهْلَهُ ثُمَّ لَنَقُولَنَّ لِوَلِيِّهِ مَا شَهِدْنَا مَهْلِكَ أَهْلِهِ وَإِنَّا لَصَادِقُونَ ﴿٤٩﴾

Wakasema: Apishaneni kwa Jina la Allaah kwamba tutamhujumu (Swaalih) kwa siri usiku na ahli yake, kisha tutasema kwa jamaa yake wa karibu: Hatukushuhudia maangamizi ya ahli yake; nasi hakika ni wa kweli.

 

 

Akaapa kila mmoja kati yao na kuchukua ahadi kwamba usiku ule, yeyote atakayeonana na Nabiy Swaalih ('alayhis-salaam) amuue. 

 

 

Lakini Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) Alimuokoa Nabiy Swaalih ('alayhis-salaam) pamoja na kuikoa aila yake na wale walioamini kwa   kuwaondosha usiku ule kwenda sehemu nyingine. Hivyo Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) Akapanga mipango Yake adhimu ya kupindua njama zao na kuzifanya njama zao ziwarudie wenyewe. 

 

Mujaahid kasema: "Wameapa kiapo na kuchukua ahadi ya kumuua lakini kabla ya hawajamfikia, wao na watu wao wakaangamizwa."

 

 

Maangamizi Ya Watu Wa Thamuwd:

 

Nabiy Swaalih ('alayhis-salaam) alikuwa ana sehemu maalumu ya kutekeleza ‘ibaada zake nayo ni katika bonde lenye mawe.  Wakasema waovu hao: “Akija Swaalih kuswali tutamuua kisha tutarudi, na tukishammaliza tutakwenda kwa aila yake na kuwamaliza nao pia.”

 

Lakini Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) Akawateremshia jiwe kubwa kutoka mlimani, wakakhofia kuwa jiwe lile litawaangukia na kuwasaga, hivyo wakakimbia katika pango lakini lile jiwe likaziba upenyo wa pango hilo hali ya kuwa wamo ndani. Watu wao hawakua na khabari hiyo ya yaliyowafika!  Anasema Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa):

 

وَمَكَرُوا مَكْرًا وَمَكَرْنَا مَكْرًا وَهُمْ لَا يَشْعُرُونَ ﴿٥٠﴾

Wakapanga njama Nasi Tukapanga mipango ya kuvurumisha njama nao huku hawatambui.

 

 

Ikawa hiyo ni moja katika adhabu za Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) kwa watu wa Thamuwd, na wengineo Akawaadhibu kwa maangamizi mengineyo kama Alivyotaja Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa):

 

وَأَخَذَ الَّذِينَ ظَلَمُوا الصَّيْحَةُ فَأَصْبَحُوا فِي دِيَارِهِمْ جَاثِمِينَ﴿٦٧﴾

Na wale waliodhulumu uliwachukuwa ukelele angamizi, wakapambazukiwa wameanguka kifudifudi majumbani mwao (wamekufa). [Huwd: 67]

 

 

Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) Akamuokoa Nabiy Swaalih ('alayhis-salaam) pamoja na wale walioamini kama Anavyosema (Subhaanahu wa Ta'aalaa): 

 

فَلَمَّا جَاءَ أَمْرُنَا نَجَّيْنَا صَالِحًا وَالَّذِينَ آمَنُوا مَعَهُ بِرَحْمَةٍ مِّنَّا وَمِنْ خِزْيِ يَوْمِئِذٍ ۗ إِنَّ رَبَّكَ هُوَ الْقَوِيُّ الْعَزِيزُ﴿٦٦﴾

Basi ilipokuja amri Yetu, Tulimuokoa Swaalih na wale walioamini pamoja naye kwa rahmah kutoka Kwetu, na kutokana na hizaya ya Siku hiyo. Hakika Rabb wako Yeye Ndiye Mwenye nguvu, Mwenye enzi ya nguvu Asiyeshindika.

 

 

وَأَخَذَ الَّذِينَ ظَلَمُوا الصَّيْحَةُ فَأَصْبَحُوا فِي دِيَارِهِمْ جَاثِمِينَ﴿٦٧﴾

Na wale waliodhulumu uliwachukuwa ukelele angamizi, wakapambazukiwa wameanguka kifudifudi majumbani mwao (wamekufa).

 

 

كَأَن لَّمْ يَغْنَوْا فِيهَا ۗ أَلَا إِنَّ ثَمُودَ كَفَرُوا رَبَّهُمْ ۗ أَلَا بُعْدًا لِّثَمُودَ﴿٦٨﴾

Kama kwamba hawakuishi wakineemeka humo. Tanabahi! Hakika kina Thamuwd walimkufuru Rabb wao. Tanabahi! Wameangamiziliwa mbali kina Thamuwd. [Huwd: 66-68]

 

 

 

Maangamizi yao yalikuwa baada ya siku tatu kama ilivyotajwa:

 

 

فَعَقَرُوهَا فَقَالَ تَمَتَّعُوا فِي دَارِكُمْ ثَلَاثَةَ أَيَّامٍ ۖ ذَٰلِكَ وَعْدٌ غَيْرُ مَكْذُوبٍ﴿٦٥﴾

Basi wakamuua; (Swaalih) akasema: Stareheni majumbani mwenu siku tatu. Hiyo ni ahadi isiyo ya uongo. [Huwd: 65]

 

Maangamizi yalianza   kuwadhihirikia kama walivyoonywa na Nabiy Swaalih ('alayhis-salaam). Nayo yalianza siku ya Alkhamys, nyuso zao zikaanza kubadilika rangi kuwa manjano.  Kisha siku ya Ijumaa zikawa nyekundu. Kisha siku ya Jumamosi nyuso zao zikageuka kuwa nyeusi kabisa. 

   

Baada ya kuchomoza jua siku ya Jumapili wakawa wanangojea wakitaja kujua ni adhabu gani hiyo itawafika ambayo Nabiy Swaalih ('alayhis-salaam) aliwaonya:

 

Ikaanza kumiminika mvua ya nguvu ya umeme na radi kisha ikafuatia mtetemeko wa ardhi mkali ambao uliharibu mji mzima na kuwaangamiza watu wake. Mji ulitingishwa na viumbe vyote vilivyokuwemo humo vilikufilia mbali. Anasema Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa):

فَأَخَذَتْهُمُ الرَّجْفَةُ فَأَصْبَحُوا فِي دَارِهِمْ جَاثِمِينَ ﴿٧٨﴾

  Basi ikawachukua tetemeko la ardhi wakawa majumbani mwao wenye kuanguka kifudifudi (wamekufa). [Al-A’raaf: 78]

 

 

Athari za adhabu za Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) kwa kaumu mbali mbali waliokanusha Rusuli wa Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) zipo bado duniani sehemu mbali mbali kwa mfano:

 

Adhabu ya watu kaumu ya Nabiy Luutw ('alayhis-salaam) ilikuwa ni bahari iliyokufa inayojulikana kwa ‘the dead sea’. Ndio maana   Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) Anasema katika Aayah kadhaa:

 

قُلْ سِيرُوا فِي الْأَرْضِ ثُمَّ انظُرُوا كَيْفَ كَانَ عَاقِبَةُ الْمُكَذِّبِينَ ﴿١١﴾

Sema: Nendeni katika ardhi, kisha mtazame vipi ilikuwa hatima ya wenye kukadhibisha. [Al-An’aam: 11]

 

 

Na Anasema pia Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa):

 

أَفَلَمْ يَسِيرُوا فِي الْأَرْضِ فَيَنظُرُوا كَيْفَ كَانَ عَاقِبَةُ الَّذِينَ مِن قَبْلِهِمْ ۚ دَمَّرَ اللَّـهُ عَلَيْهِمْ ۖ وَلِلْكَافِرِينَ أَمْثَالُهَا﴿١٠﴾

Je, hawakutembea katika ardhi wakatazama vipi imekuwa hatima ya ambao wa kabla yao? Allaah Amewadamirisha mbali, na kwa makafiri (itakuwa) mfano wa hayo. [Muhammad: 10]

 

Na Anasema Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) maangamizi ya kaumu ya Thamuwd:

 

فَانظُرْ كَيْفَ كَانَ عَاقِبَةُ مَكْرِهِمْ أَنَّا دَمَّرْنَاهُمْ وَقَوْمَهُمْ أَجْمَعِينَ ﴿٥١﴾

Basi tazama vipi ilikuwa hatima ya njama zao, kwamba Tuliwadamirisha na watu wao wote.

 

فَتِلْكَ بُيُوتُهُمْ خَاوِيَةً بِمَا ظَلَمُوا ۗ إِنَّ فِي ذَٰلِكَ لَآيَةً لِّقَوْمٍ يَعْلَمُونَ ﴿٥٢﴾

Basi hizo ni nyumba ni magofu kwa sababu ya yale waliyodhulumu. Hakika katika hayo kuna Aayah (ishara, zingatio, funzo n.k.) kwa watu wanaojua. [An-Naml: 51-52]

 

 

Vile vile Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) Kataja adhabu yao nyingine ya ukelele mkali ambao kabla ya kumalizika kwake ukelele huo, makafiri wote wa Thamuwd walikufa pamoja wote kwa wakati mmoja.  Hakuna chochote kilichoweza kuwahifadhi, wala majumba yao ya mawe na ya kifakhari ya   hayakuweza kuwalinda na adhabu hizo: Anasema Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa):

 

وَأَخَذَ الَّذِينَ ظَلَمُوا الصَّيْحَةُ فَأَصْبَحُوا فِي دِيَارِهِمْ جَاثِمِينَ﴿٦٧﴾

Na wale waliodhulumu uliwachukuwa ukelele angamizi, wakapambazukiwa wameanguka kifudifudi majumbani mwao (wamekufa).

 

 

 

كَأَن لَّمْ يَغْنَوْا فِيهَا ۗ أَلَا إِنَّ ثَمُودَ كَفَرُوا رَبَّهُمْ ۗ أَلَا بُعْدًا لِّثَمُودَ﴿٦٨﴾

Kama kwamba hawakuishi wakineemeka humo. Tanabahi! Hakika kina Thamuwd walimkufuru Rabb wao. Tanabahi! Wameangamiziliwa mbali kina Thamuwd. [Huwd: 67-68]

 

 

Na Anasema pia Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) kuhusu adhabu za kaumu ya Thamuwd:

 

 

وَأَمَّا ثَمُودُ فَهَدَيْنَاهُمْ فَاسْتَحَبُّوا الْعَمَىٰ عَلَى الْهُدَىٰ فَأَخَذَتْهُمْ صَاعِقَةُ الْعَذَابِ الْهُونِ بِمَا كَانُوا يَكْسِبُونَ﴿١٧﴾

Na ama kina Thamuwd, Tuliwaongoza, lakini walistahabu upofu kuliko Uongofu basi ikawachukuwa radi na umeme angamizi wa adhabu idhalilishayo kwa yale waliyokuwa wakichuma.

 

وَنَجَّيْنَا الَّذِينَ آمَنُوا وَكَانُوا يَتَّقُونَ﴿١٨﴾

Na Tukawaokoa wale walioamini na walikuwa wenye taqwa. [Fusw-Swilat: 17-18]

 

 

Na Anasema pia Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa):

 

كَذَّبَتْ ثَمُودُ وَعَادٌ بِالْقَارِعَةِ﴿٤﴾

Kina Thamuwd na ‘Aad walikadhibisha tukio lenye kugongagonga na kutia kiwewe nyoyo.

 

فَأَمَّا ثَمُودُ فَأُهْلِكُوا بِالطَّاغِيَةِ﴿٥﴾

Ama kina Thamuwd, waliangamizwa kwa ukelele mkali uliovuka mipaka. [Al-Haaqah: 4-5]

 

 

Maelezo zaidi kuhusu adhabu za kaumu ya Thamuwd:

 

فَكَيْفَ كَانَ عَذَابِي وَنُذُرِ ﴿٣٠﴾

Basi vipi ilikuwa adhabu Yangu na maonyo Yangu?

 

 

إِنَّا أَرْسَلْنَا عَلَيْهِمْ صَيْحَةً وَاحِدَةً فَكَانُوا كَهَشِيمِ الْمُحْتَظِرِ ﴿٣١﴾

Hakika Sisi Tumewapelekea ukelele angamizi mmoja tu, basi wakawa kama mabuwa yaliyokatika-katika ya mtengenezaji zizi. [Al-Qamar: 30-31]

 

As-Sudi kasema: “Walikuwa kama nyasi kavu za kichaka katika jangwa,  zinapoungua na kupeperushwa na upepo.”  

 

Ibn Zayd kasema "Waarabu walikuwa wakisimamisha 'Hizar' (kutokana na neno 'almuhtazir') ambayo ni kichaka kikavu, (walichowazungushia) wakiwawekea ngamia na ngo'mbe. Ndipo Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa)   Aliposema:

 

  فَكَانُوا كَهَشِيمِ الْمُحْتَظِرِ ﴿٣١﴾

Basi wakawa kama mabuwa yaliyokatika-katika ya mtengenezaji zizi. [Al-Qamar: 31]

 

 

Na pia kauli za Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) kuhusu kaumu ya Thamuwd:

 

 

كَذَّبَتْ ثَمُودُ الْمُرْسَلِينَ ﴿١٤١﴾

Kina Thamuwd walimkadhibisha Rusuli.

 

 

إِذْ قَالَ لَهُمْ أَخُوهُمْ صَالِحٌ أَلَا تَتَّقُونَ ﴿١٤٢﴾

Alipowaambia ndugu yao Swaalih: Je, hamtokuwa na taqwa?

 

 

إِنِّي لَكُمْ رَسُولٌ أَمِينٌ ﴿١٤٣﴾

Hakika mimi kwenu ni Rasuli mwaminifu.

 

 

فَاتَّقُوا اللَّـهَ وَأَطِيعُونِ ﴿١٤٤﴾

Basi mcheni Allaah na nitiini.

 

 

وَمَا أَسْأَلُكُمْ عَلَيْهِ مِنْ أَجْرٍ ۖ إِنْ أَجْرِيَ إِلَّا عَلَىٰ رَبِّ الْعَالَمِينَ ﴿١٤٥﴾

Na wala sikuombeni ujira wowote juu yake.  Ujira wangu hauko isipokuwa kwa Rabb wa walimwengu.

 

أَتُتْرَكُونَ فِي مَا هَاهُنَا آمِنِينَ ﴿١٤٦﴾

Je, mtaachwa mkiwa katika amani kwenye haya hapa mliyonayo? 

 

 

فِي جَنَّاتٍ وَعُيُونٍ ﴿١٤٧﴾

Katika mabustani na chemchemu.

 

 

وَزُرُوعٍ وَنَخْلٍ طَلْعُهَا هَضِيمٌ ﴿١٤٨﴾

Na mimea na mitende makole yake laini, yamewiva.

 

 

وَتَنْحِتُونَ مِنَ الْجِبَالِ بُيُوتًا فَارِهِينَ ﴿١٤٩﴾

Na mnachonga majabalini nyumba kwa uhodari kabisa.

 

 

فَاتَّقُوا اللَّـهَ وَأَطِيعُونِ ﴿١٥٠﴾

Basi mcheni Allaah na nitiini.

 

 

وَلَا تُطِيعُوا أَمْرَ الْمُسْرِفِينَ ﴿١٥١﴾

Na wala msitii amri ya wenye kupindukia mipaka.

 

 

الَّذِينَ يُفْسِدُونَ فِي الْأَرْضِ وَلَا يُصْلِحُونَ ﴿١٥٢﴾

Ambao wanafanya ufisadi katika ardhi na wala hawatengenezi.

 

 

قَالُوا إِنَّمَا أَنتَ مِنَ الْمُسَحَّرِينَ ﴿١٥٣﴾

Wakasema: Hakika wewe ni miongoni mwa waliorogwa.

 

 

مَا أَنتَ إِلَّا بَشَرٌ مِّثْلُنَا فَأْتِ بِآيَةٍ إِن كُنتَ مِنَ الصَّادِقِينَ ﴿١٥٤﴾

Wewe si chochote isipokuwa mtu kama sisi; basi lete Aayah (dalili, muujiza) ukiwa wewe ni miongoni mwa wakweli.

 

 

قَالَ هَـٰذِهِ نَاقَةٌ لَّهَا شِرْبٌ وَلَكُمْ شِرْبُ يَوْمٍ مَّعْلُومٍ ﴿١٥٥﴾

Akasema: Huyu hapa ngamia jike ana zamu ya kinywaji, nanyi mna zamu ya kinywaji siku maalumu.

 

 

وَلَا تَمَسُّوهَا بِسُوءٍ فَيَأْخُذَكُمْ عَذَابُ يَوْمٍ عَظِيمٍ ﴿١٥٦﴾

Na wala msimguse kwa uovu, ikaja kukuchukueni adhabu ya Siku adhimu.

 

 

فَعَقَرُوهَا فَأَصْبَحُوا نَادِمِينَ ﴿١٥٧﴾

Basi wakamuua wakapambazukiwa wenye kujuta.

 

 

فَأَخَذَهُمُ الْعَذَابُ ۗ إِنَّ فِي ذَٰلِكَ لَآيَةً ۖ وَمَا كَانَ أَكْثَرُهُم مُّؤْمِنِينَ ﴿١٥٨﴾

Ikawachukuwa adhabu. Hakika katika hayo pana Aayah (ishara, zingatio n.k.), lakini wengi wao hawakuwa wenye kuamini. [Ash-Shu’araa: 141-158]

 

 

Maelezo zaidi ya kisa cha watu wa Thamuwd katika kauli za Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa):

 

كَذَّبَتْ ثَمُودُ بِالنُّذُرِ ﴿٢٣﴾

Kina Thamuwd waliwakadhibisha Waonyaji.

 

 

فَقَالُوا أَبَشَرًا مِّنَّا وَاحِدًا نَّتَّبِعُهُ إِنَّا إِذًا لَّفِي ضَلَالٍ وَسُعُرٍ ﴿٢٤﴾

Wakasema: Ah! Tumfuate binaadamu miongoni mwetu? Hakika hapo sisi tutakuwa katika upotofu na wazimu. 

 

أَأُلْقِيَ الذِّكْرُ عَلَيْهِ مِن بَيْنِنَا بَلْ هُوَ كَذَّابٌ أَشِرٌ ﴿٢٥﴾

Ah! Ameteremshiwa ukumbusho baina yetu? Bali yeye ni muongo mkubwa mfidhuli mwenye kutakabari mno.

 

سَيَعْلَمُونَ غَدًا مَّنِ الْكَذَّابُ الْأَشِرُ ﴿٢٦﴾

Watakuja kujua kesho nani muongo mkubwa mfidhuli mwenye kutakabari mno.

 

 

إِنَّا مُرْسِلُو النَّاقَةِ فِتْنَةً لَّهُمْ فَارْتَقِبْهُمْ وَاصْطَبِرْ ﴿٢٧﴾

Hakika Sisi Tutawapelekea ngamia jike awe jaribio kwao, basi (ee Nabiy Swaalih   عليه السلام) watazame na vuta subira.

 

وَنَبِّئْهُمْ أَنَّ الْمَاءَ قِسْمَةٌ بَيْنَهُمْ ۖ كُلُّ شِرْبٍ مُّحْتَضَرٌ ﴿٢٨﴾

Na wajulishe kwamba maji ni mgawanyo baina yao (ngamia na wao), kila sehemu ya maji itahudhuriwa (kwa zamu).

 

فَنَادَوْا صَاحِبَهُمْ فَتَعَاطَىٰ فَعَقَرَ ﴿٢٩﴾

Wakamwita swahibu wao, akakamata (upanga) akaua (ngamia).

 

فَكَيْفَ كَانَ عَذَابِي وَنُذُرِ ﴿٣٠﴾

Basi vipi ilikuwa adhabu Yangu na maonyo Yangu?

 

 

إِنَّا أَرْسَلْنَا عَلَيْهِمْ صَيْحَةً وَاحِدَةً فَكَانُوا كَهَشِيمِ الْمُحْتَظِرِ ﴿٣١﴾

Hakika Sisi Tumewapelekea ukelele angamizi mmoja tu, basi wakawa kama mabuwa yaliyokatika-katika ya mtengenezaji zizi. [Al-Qamar: 23-31]

 

 

Na katika Suwrah Huwd:

 

 

وَإِلَىٰ ثَمُودَ أَخَاهُمْ صَالِحًا ۚ قَالَ يَا قَوْمِ اعْبُدُوا اللَّـهَ مَا لَكُم مِّنْ إِلَـٰهٍ غَيْرُهُ ۖ هُوَ أَنشَأَكُم مِّنَ الْأَرْضِ وَاسْتَعْمَرَكُمْ فِيهَا فَاسْتَغْفِرُوهُ ثُمَّ تُوبُوا إِلَيْهِ ۚ إِنَّ رَبِّي قَرِيبٌ مُّجِيبٌ﴿٦١﴾

Na kwa Thamuwd (Tulimpeleka) ndugu yao Swaalih. Akasema: Enyi kaumu yangu! Mwabuduni Allaah, hamna mwabudiwa wa haki ghairi Yake. Yeye Ndiye Aliyekuanzisheni katika ardhi, na Akakufanyieni makazi humo; basi mwombeni maghfirah, kisha tubieni Kwake. Hakika Rabb wangu Yuko Karibu kwa ujuzi Wake, Mwenye kuitikia.

 

 

قَالُوا يَا صَالِحُ قَدْ كُنتَ فِينَا مَرْجُوًّا قَبْلَ هَـٰذَا ۖ أَتَنْهَانَا أَن نَّعْبُدَ مَا يَعْبُدُ آبَاؤُنَا وَإِنَّنَا لَفِي شَكٍّ مِّمَّا تَدْعُونَا إِلَيْهِ مُرِيبٍ﴿٦٢﴾

Wakasema: Ee Swaalih! Kwa yakini ulikuwa kwetu mwenye kutarajiwa (khayr) kabla ya haya. Je, unatukataza kuabudu wale wanaowaabudu baba zetu; na hakika sisi tumo katika shaka na wasiwasi katika unayotuitia.

 

 

قَالَ يَا قَوْمِ أَرَأَيْتُمْ إِن كُنتُ عَلَىٰ بَيِّنَةٍ مِّن رَّبِّي وَآتَانِي مِنْهُ رَحْمَةً فَمَن يَنصُرُنِي مِنَ اللَّـهِ إِنْ عَصَيْتُهُ ۖ فَمَا تَزِيدُونَنِي غَيْرَ تَخْسِيرٍ﴿٦٣﴾

 (Swaalih) Akasema: Enyi kaumu yangu! Je, mnaonaje ikiwa niko katika hoja bayana kutoka kwa Rabb wangu, na Amenipa rahmah (Unabiy na risala) kutoka Kwake basi nani atakayeninusuru nikimuasi? Basi hamnizidishii ila khasara.

 

 

وَيَا قَوْمِ هَـٰذِهِ نَاقَةُ اللَّـهِ لَكُمْ آيَةً فَذَرُوهَا تَأْكُلْ فِي أَرْضِ اللَّـهِ وَلَا تَمَسُّوهَا بِسُوءٍ فَيَأْخُذَكُمْ عَذَابٌ قَرِيبٌ﴿٦٤﴾

Enyi kaumu yangu! Huyu ni ngamia jike wa Allaah, ni Aayah (miujiza, ishara) kwenu, basi mwacheni ale katika ardhi ya Allaah, na wala msimguse kwa uovu ikakupateni adhabu iliyo karibu.

 

فَعَقَرُوهَا فَقَالَ تَمَتَّعُوا فِي دَارِكُمْ ثَلَاثَةَ أَيَّامٍ ۖ ذَٰلِكَ وَعْدٌ غَيْرُ مَكْذُوبٍ﴿٦٥﴾

Basi wakamuua; (Swaalih) akasema: Stareheni majumbani mwenu siku tatu. Hiyo ni ahadi isiyo ya uongo.

 

 

فَلَمَّا جَاءَ أَمْرُنَا نَجَّيْنَا صَالِحًا وَالَّذِينَ آمَنُوا مَعَهُ بِرَحْمَةٍ مِّنَّا وَمِنْ خِزْيِ يَوْمِئِذٍ ۗ إِنَّ رَبَّكَ هُوَ الْقَوِيُّ الْعَزِيزُ﴿٦٦﴾

Basi ilipokuja amri Yetu, Tulimuokoa Swaalih na wale walioamini pamoja naye kwa rahmah kutoka Kwetu, na kutokana na hizaya ya Siku hiyo. Hakika Rabb wako Yeye Ndiye Mwenye nguvu, Mwenye enzi ya nguvu Asiyeshindika.

 

وَأَخَذَ الَّذِينَ ظَلَمُوا الصَّيْحَةُ فَأَصْبَحُوا فِي دِيَارِهِمْ جَاثِمِينَ﴿٦٧﴾

Na wale waliodhulumu uliwachukuwa ukelele angamizi, wakapambazukiwa wameanguka kifudifudi majumbani mwao (wamekufa).

 

 

كَأَن لَّمْ يَغْنَوْا فِيهَا ۗ أَلَا إِنَّ ثَمُودَ كَفَرُوا رَبَّهُمْ ۗ أَلَا بُعْدًا لِّثَمُودَ﴿٦٨﴾

Kama kwamba hawakuishi wakineemeka humo. Tanabahi! Hakika kina Thamuwd walimkufuru Rabb wao. Tanabahi! Wameangamiziliwa mbali kina Thamuwd.  [Huwd: 61-68]

 

 

 

Athari Za Maangamizi Ya Kaumu Ya Thamuwd Zingalipo Duniani:

 

 

Ibn 'Umar (Radhwiya Allaahu ‘anhumaa) amesimulia kwamba Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) alipokuwa akipita nyumba za kaumu ya Thamuwd  wakati akielekea na jeshi lake la Maswahaba kwenda  katika vita vya Tabuwk,  alisimama hapo, kisha Maswahaba wakachota maji katika visima ambavyo watu wa Thamuwd walikuwa wakichota maji. Wakatumia maji kukandia unga wao wa kupikia mikate, na wakajaza maji ya kunywa katika mifuko yao ya ngozi (viriba). Lakini Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam)  aliwaamrisha  wayamwage maji  na unga waliokanda walishe ngamia wao. Kisha akaondoka nao mpaka wakafika katika kisima ambacho ngamia wa Thamuwd alikuwa akinywa maji, akawaonya wasiingie kwa watu walioangamizwa  kwa kuwaambia: "Nakhofu  msije kupatwa  yale yaliyowapata wao, kwa hiyo msiingie kwao."

 

Riwaayah nyingine imesema:

 

عن عبد الله بن عمر قال: قال رسول الله صلى الله عليه وسلم وهو بالحجر: ((لا تدخلوا على هؤلاء المعذبين، إلا أن تكونوا باكين، فإن لم تكونوا باكين فلا تدخلوا عليهم، أن يصيبكم مثل ما أصابهم)). أخرجاه في (الصحيحين) من غير وجه.

Abdullaah Bbin 'Amr amehadithia: Rasuli wa Allaah (صلى الله عليه وآله وسلم) amesema pindi alipokuwa Hijr  "Msiingie kwao hawa walioadhibiwa, isipokuwa muingie na huku mnalia, na kama hamlii basi msiingie kwao msije kufikwa na masaibu kama yaliyowafikia wao)) [Al-Bukhari na Muslim]

 

Na Allaah Anajua zaidi

 

 لَقَدْ كَانَ فِي قَصَصِهِمْ عِبْرَةٌ لِّأُولِي الْأَلْبَابِ ۗ مَا كَانَ حَدِيثًا يُفْتَرَىٰ وَلَـٰكِن تَصْدِيقَ الَّذِي بَيْنَ يَدَيْهِ وَتَفْصِيلَ كُلِّ شَيْءٍ وَهُدًى وَرَحْمَةً لِّقَوْمٍ يُؤْمِنُونَ ﴿١١١﴾

Kwa yakini katika visa vyao kuna mafunzo kwa wenye akili. Haikuwa (Qur-aan) hadithi zinazotungwa, lakini ni sadikisho la (vitabu) vya kabla yake na tafsili ya waziwazi ya kila kitu, na ni mwongozo na rahmah kwa watu wanaoamini. [Yuwsuf: 111]

 

 

Share