026-Swahiyh Fiqh As-Sunnah: Mlango Wa Twahara: Fadhila Za Wudhuu

 

Swahiyh Fiqh As-Sunnah

 

Mlango Wa Twahara

 

026-Fadhla Za Wudhuu

 

Alhidaaya.com

 

 

 

1- Ni kama nusu ya iymaan:

 

 

Ni kama katika Hadiyth ya Abuu Maalik Al-Ash‘ariy (Radhi za Allaah ziwe juu yake) aliyesema: “Rasuli (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) anasema:

 

((الطهور شطر الايمان))                  

                             

((Twahara ni nusu ya iymaan)). [Hadiyth Swahiyh. Imefanyiwa “ikhraaj” na Muslim (223) na wengineo.]

 

 

2- Hufuta madhambi madogo madogo:

 

 

(a) Imepokelewa toka kwa Abuu Hurayrah (Radhi za Allaah ziwe juu yake) kwamba Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) amesema:

 

((إذا توضأ العبد المسلمأو المؤمنفغسل وجهه خرج من وجهه كل خطيئة نظر إليها مع قطر الماءأو مع آخر قطر الماء-، فإذا غسل يديه خرجت من يديه كل خطيئة كان بطشتها يداه مع الماءأو مع آخر قطر الماءفإذا غسل رجليه خرجت كل خطيئة مشتها رجلاه مع الماءأو مع آخر قطر الماءحتى يخرج نقيا من الذنوب))   

 ((Anapotawadha mja Muislamu – au Muumini – akauosha uso wake, hutoka katika uso huo pamoja na matone ya maji kila kosa la kuangalia – au pamoja na tone la mwisho la maji - , na anapoosha mikono yake miwili, hutoka katika mikono hiyo pamoja na maji, kila kosa ambalo mikono yake imetumilia nguvu – au pamoja na tone la mwisho la maji - , na anapoosha miguu yake miwili, hutoka pamoja na maji kila kosa ambalo miguu yake ililiendea – au pamoja na tone la mwisho la maji, mpaka hutoka akiwa ametakasika kabisa na madhambi)). [Hadiyth Swahiyh. Imefanyiwa “ikhraaj” na Muslim (244) na wengineo].

 

(b) Imepokelewa toka kwa ‘Uthmaan (Radhi za Allaah ziwe juu yake) kwamba Rasuli (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) amesema: 

 

((من توضأ هكذا غفر له ما تقدم من ذنبه، وكانت صلاته ومشيه إلى المسجد نافلة))    

((Mwenye kutawadha hivi, husamehewa dhambi zake zilizopita, na Swalaah yake na kwenda kwake Msikitini huwa ni thawabu ziada. [Hadiyth Swahiyh. Imefanyiwa “ikhraaj” na Muslim (229) na wengineo].

 

 

Fadhila na thawabu hizi hupatikana kwa uhakika zaidi kwa mwenye kuswali moja kwa moja Swalaah ya faradhi au ya Sunnah baada ya kutawadha.

 

(c) Katika Hadiyth ya ‘Uthmaan akizungumzia namna wudhuu wa Rasuli (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) ulivyo, anasema: “Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) anasema:

 

((من توضأ مثل وضوئي هذا ثم قام فصلى ركعتين لا يحدث فيهما نفسه، غفر له ما تقدم من ذنبه)) 

((Mwenye kutawadha kama ninavyotawadha mimi hivi, kisha akasimama akaswali rakaa mbili, haizungumzishi nafsi yake ndani yake, ila hufutiwa dhambi zake zilizotangulia)). [Hadiyth Swahiyh. Imefanyiwa “ikhraaj” na Al-Bukhaary (6433), Muslim (226) na wengineo].

 

 

3- Hunyanyua daraja za mja:

 

Imepokelewa toka kwa Abu Hurayrah (Radhi za Allaah ziwe juu yake) kwamba Rasuli (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) amesema:

((ألا أدلكم على ما يمحو الله به الخطايا ويرفع به الدرجات؟)) قالوا: بلى يا رسول الله! قال: ((إسباغ الوضوء على المكاره، وكثرة الخطا إلى المساجد، وانتظار الصلاة بعد الصلاة، فذلكم الرباط، فذلكم الرباط، فذلكم الرباط))

((Je, niwaambieni lile ambalo kwalo Allaah Huyafuta makosa na Hunyanyua kwalo daraja? Wakasema: “Tuambie, ee Rasuli wa Allaah! Akasema: Kutawadha kikamilifu pamoja na kuwepo uzito na ugumu, kukithirisha hatua kwenda Msikitini, na kusubiri Swalaah baada ya Swalaah, basi hayo ni mambo ya mtu kujifunga nayo, basi hayo ni mambo ya mtu kujifunga nayo, basi hayo ni mambo ya mtu kujifunga nayo)). [Hadiyth Swahiyh. Imefanyiwa “ikhraaj” na Muslim (251) na wengineo].

 

 

4- Ni njia ya kuelekea peponi:

 

(a) Imepokelewa toka kwa Abu Hurayrah (Radhi za Allaah iwe juu yake) kwamba Rasuli (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) alimwambia Bilaal: 

 

(( يا بلال! حدثني بأرجى عمل عملته فى الاسلام، إني سمعت دف نعليك بين يدي في الجنة)). قال : ((ماعملت عملا أرجى عندي من أني لم أتطهر طهورا في ساعة من ليل أو نهار إلا صليت بذلك الطهور ما كتب لي أن أصلى))

((Ee Bilaal! Nielezee amali yenye matarajio zaidi uliyoifanya katika Uislamu, kwani mimi nimesikia mtaharuki wa viatu vyako mbele yangu huko peponi)).

Bilaal akasema: “Sikufanya amali yoyote yenye matarajio makubwa kwangu zaidi ya kuwa sikupata kujitwaharisha wakati wowote wa usiku au mchana, ila huswali kwa twahara hiyo kile nilichoandikiwa kukiswali”. [Hadiyth Swahiyh. Imefanyiwa “ikhraaj” na Al-Bukhaary (1149), Muslim (2458) na wengineo].

 

 

(b) Imepokelewa toka kwa ‘Uqbah bin ‘Aamir (Radhi za Allaah ziwe juu yake) akisema: “Nimemsikia Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) akisema: 

 

((من توضأ فأحسن الوضوء ثم صلى ركعتين، يقبل عليهما بقلبه ووجهه، وجبت له الجنة))

((Mwenye kutawadha, akaukamilisha vyema wudhuu wake kama inavyotakikana, kisha akaswali rakaa mbili, akafanya khushui kwa moyo wake na uso wake (viungo vyake), basi ni lazima aingie peponi)). [Hadiyth Swahiyh. Imefanyiwa “ikhraaj” na Muslim (234) An-Nasaaiy (1/80) na wengineo].

 

 

(5) Utakuwa ni alama itakayoupambanua Ummah huu wakati wa kupita kwenye hawdh:

 

 

Imepokelewa toka kwa Abu Hurayrah (Radhi za Allaah ziwe juu yake) kwamba Rasuli (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) alikwenda makaburini akasema:

 

((السلام عليكم دار قوم مؤمنين وإنا- إن شاء الله- بكم عن قريب لاحقون، وددت لو أنا قد رأينا إخواننا)) قالوا: أو لسنا إخوانك يا رسول الله؟ قال: ((أنتم أصحابي، وإخواننا الذين لم يأتوا بعد)) فقالوا: كيف تعرف من لم يأت من أمتك يا رسو ل الله؟ قال: (( أرأيت لو أن رجلا له خيل غر محجلة بين ظهري خيل دهم بهم ألا يعرف خيله؟)) قالوا: بلى يا رسول الله، قال: ((فإنهم يأتون غرا محجلين من الوضوء، وأنا فرطهم على الحوض، ألا ليذادن رجال عن حوضى كما يذاد البعير الضال أناديهم ألا هلم فيقال: إنهم قد بدلوا بعدك، فأقول:  سحقا سحقا))

                                                                                                        

((Amani iwe juu yenu nyumba ya jamaa ya Waumini. Na sisi bila shaka Apendapo Allaah tutakuwa nanyi hivi karibuni. Ningependa lau sisi tungeliwaona ndugu zetu)). Wakasema: “Ee Rasuli wa Allaah! Je, sisi sio ndugu zako”? Akasema:

((Nyinyi ni Maswahaba zangu. Ama ndugu zangu, hao ni wale ambao hawajakuja bado)). Wakasema: “Ni vipi utamtambua yule ambaye bado hajakuja katika umati wako ee Rasuli wa Allaah?”. Akasema: ((Niambieni, lau kama mtu ana farasi wenye alama usoni na miguuni wakawa baina ya farasi weusi wasio na mabaka, je hawezi kuwatambua farasi wake?)).  Wakasema: “Ndio, atawatambua ee Rasuli wa Allaah”. Akasema:  ((Basi wao watakuja nailhali wana nuru nyusoni, miguuni na mikononi kutokana na wudhuu. Na mimi ndiye nitakayewatangulia kwenye hawdh. Basi jueni kwa yakini kwamba watu watazuiliwa na kufukuzwa wasije kwenye hawdh langu kama wanavyozuiliwa ngamia wasio na mchunga. Nitawaita: Haya njooni! Patasemwa: “Hakika hao walibadili baada yako”. Nitawaambia: Poteleeni mbali kabisa)).[Hadiyth Swahiyh. Imefanyiwa “ikhraaj” na Muslim (234), An-Nasaaiy (1/80) na wengineo].

 

 

(6) Ni nuru kwa mja siku ya Qiyaamah:

 

Imepokelewa toka kwa Abu Hurayrah (Radhi za Allaah ziwe juu yake) akisema: “Nimemsikia Kipenzi changu (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) akisema:

 

 ((تبلغ الحلية من المؤمنين حيث يبلغ  الوضوء))  

((Nuru ya Waumini itafikilia pale wudhuu unapofikilia)).

 

 

 

(7) Unafungua kifundo cha shaytwaan:

 

Imepokelewa toka kwa Abuu Hurayrah (Radhi za Allaah ziwe juu yake) kwamba Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) amesema: 

 

((يعقد الشيطان على قافية رأس أحدكم إذا هو نام ثلاث عقد يضرب كل عقدة: عليك ليل طويل فارقد، فإن استيقظ فذكر الله انحلت عقدة، فإن توضأ انحلت عقدة، فإن صلى انحلت عقدة، فأصبح نشيطا طيب النفس،   وإلا أصبح خبيث النفس كسلان))                                           

((Anapolala mmoja wenu, shaytwaan hufunga kisogoni mwake vifundo vitatu. Hupiga kila kifundo (kumwambia): Umebakiwa na usiku mrefu, basi lala. Anapoamka akamtaja Allaah, kifundo kimoja hufunguka. Anapotawadha, hufunguka kingine, na anaposwali cha tatu hufunguka. Hapo huwa mchangamfu na mwenye nafsi nzuri, na kama si hivyo, huwa na nafsi mbaya na mvivu)).[Hadiyth Swahiyh. Imefanyiwa “ikhraaj” na Al-Bukhaary (1142) na Muslim (776)].

 

 

 

Share