Kuingia Peponi Mtu Anayetoa Shahada Kabla Ya Kufa

 

Kuingia Peponi Mtu Anayetoa Shahada Kabla Ya Kufa

 

Alhidaaya.com

 

 

SWALI:

 

According to the Sunnah (I am not exactly certain which hadith) it is stated that whoever says Shahada on the death bed or while dying is going to Jannah! What is exactly means by this? Does it mean anybody who says Shahada during the last seconds of his life will go to Paradise? Please enlighten me.

Shukran.

 

* A Swahili answer is ok too - samahani kuandika kiengereza

 

 

JIBU:

 

AlhamduliLLaah - Himidi Anastahiki Allaah (Subhaanahu wa Ta’aala) Rabb wa walimwengu, Swalaah na Salaam zimshukie Nabiy Muhammad (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) na Swahaba zake (Radhwiya Allaahu 'anhum) na waliowafuata kwa wema mpaka Siku ya Mwisho

 

Kwa uwezo wa Allaah Aliyetukuka tutajaribu kukufahamisha hilo. Ni muhimu kuelewa kuwa mwanzo wa yote inatakiwa kuwa maneno ya kwanza anayoyasikia mtoto anapokuja ulimwenguni ni kauli hiyo ya kumpwekesha Allaah (Subhaanahu wa Ta‘aalaa). Hili ni kwa mujibu ya kauli ya Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam):

 

"Wafungulieni kalimah ya kwanza kwa watoto wenu na Laa ilaaha illa Allaah" [al-Haakim kutoka kwa Ibn ‘Abbaas [Radhwiya Allaahu ‘Anhuma]). Pia kumuadhinia kwenye sikio lake la kuume ambamo ndani yake kuna kumpwekesha Allaah (Subhaanahu wa Ta‘aalaa).

 

Ama kuhusu kalimah ya mwisho ikiwa ni kauli ya Laa ilaaha illa Allaah mwenye kuisema ataingia Jannah (Peponi)  basi ipo Hadiyth iliyo sahihi. Imepokewa kwa Mu‘aadh bin Jabal (Radhwiya Allaahu ‘anhu) kuwa Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) amesema:

 

"Yeyote ambaye maneno yake ya mwisho yatakuwa ni Laa ilaaha illa Allaah ataingia Peponi" [Ahmad, Abu Daawuud na al-Haakim, na akasema Isnadi yake ni sahihi, na imesahihishwa na al-Albaaniy na Shu‘ayb al-Arna’uutw amesema ni Hasan].

 

Ndio Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) akatuusia sana tuwe ni wenye kumlakinia kwa kumkumbusha pole pole awe ni mwenye kutamka kalimah hiyo kama alivyopokea Abu Sa‘iyd al-Khudriy (Radhwiya Allaahu ‘anhu) kuwa Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) amesema:

 

"Walakinieni maiti zenu kwa Laa ilaaha illa Allaah" (Muslim, Abu Daawuud, at-Tirmidhiy na an-Nasaa’iy).

 

Kuwalikinia maiti zenu ina maana ya wanapokuwa katika kutokwa roho siyo baada ya kuaga dunia.

 

Uhakika wa Hadiyth hiyo ni kuwa yeyote anayetamka shahada kabla ya kuaga dunia basi huyo ataingia Peponi kama tulivyotaja Hadiyth hapo juu ya Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) ambaye ni msema kweli wa kusadikika. Huenda tukaona hilo ni jepesi sana lakini si rahisi kupatikana hilo kama tunavyofikiria sisi. Vipo visa vingi vya watu ambao wameshindwa kutamka shahada wakati wa kutokwa na roho mbali ya kuwa wao ni Waislamu wa kuzaliwa au kuingia katika Uislamu. Kwa yule ambaye hakuishi na Qur-aan na maagizo ya Allaah (Subhaanahu wa Ta‘aalaa) na Nabiy Wake (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) basi jambo hilo huwa gumu. Sababu kubwa ni kuwa wakati huo huwa amesimamiwa na Malaika wa kutoa roho (Malakul Mawt) anayetisha kwa kiasi hata roho yake inatolewa kwa nguvu sana. Wapo wengi waliokuwa wanaaga dunia na wanakumbushwa waseme kalimah hiyo lakini badala yake wanaimba nyimbo walizokuwa wakiimba hapa duniani au kushindwa kusema chochote.

 

Hivyo tusighurike kwa kuwa wakati huu twaweza kuisema kalimah hiyo bila matatizo yoyote wakati huo mambo yatakuwa tofauti kabisa. Ikiwa tunataka tusipate shida wakati huo inafaa tuwe ni Waislamu wa kweli wenye kufuata maagizo ya Allaah (Subhaanahu wa Ta‘aalaa) na Nabiy Wake (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam). Tukifanya hivyo tutakuwa na maisha ya sahali hapa duniani na wala hatutakuwa na maisha ya dhiki Kesho Aakhirah.

 

Tunamuomba Allaah Aliyetukuka Atujaalie ni wenye kufuata mema na mazuri na kuwa na hima katika kuyaacha yaliyo mabaya na Aturehemu pamoja na kutujaalia kuweza kutamka shahada wakati wa kufa kwetu, Aamiyn.

 

 

Na Allaah Anajua zaidi

 

Share