Kulisha Masikini Sitini

 

Kulisha Masikini Sitini

 

Alhidaaya.com

 

 

Swali:

 

Asalamu Alaykum,

 

Ikiwa mtu analisha masikini 60 jee mtu huyo anakuwa kafanya nini mbele ya Allaah? Naomba ufafanuzi wako

 

 

Jibu:

 

AlhamduliLLaah - Himidi Anastahiki Allaah (Subhaanahu wa Ta’aalaa) Rabb wa walimwengu, Swalaah na salamu zimshukie Nabiy Muhammad (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) na Swahaba zake (Radhwiya Allaahu 'anhum) na waliowafuata kwa wema mpaka Siku ya Mwisho.

 

 

Amma ba'ad,

 

Kulisha masikini kwa idadi yoyote ni amali njema na Allaah Subhaanahu wa Ta'aalaa Amesisitiza sana katika Qur-aan kulisha masikini na atakayefanya hivyo basi atapata thawaabu zake.  

 

Ama idadi ya kulisha masikini 60 haikutajwa kuwa khaswa ina fadhila fulani ila tu imekuja hukumu  ya Kafara ya 'Adh-Dhwihaar' ambayo inatoka katika neno la 'Adh-Dhwahr' yaani mgongo. Ilikuwa katika zama za Jaahiliyyah (zama za ujinga, kabla ya Uislamu) mume humuambia mkewe "Umekuwa kwangu kama mgongo wa mama yangu". Na ilikuwa ndio njia mojawapo ya kutoa Talaka wakati huo.Na Allaah Subhaanahu wa Ta'aalaa Ameruhusu Ummah huu wa Kiisalmu kulipa Kafara kwa kauli hii na haihesabiki kama ni talaka kinyume na ilivyo katika Ujaahiliyyah.

 

Kafara hii imetajwa katika aayah zifautazo ambazo ziliteremshwa baada ya Bibi Khuwaylah bint Tha'alabah kumshtakia Nabiy( Swalla Allaahu 'alayhi wa sallam) kwamba mumewe 'Aws bin As-Swaamit amemwambia kauli hiyo ya Adh-Dhwihaar :

 

قَدْ سَمِعَ اللَّـهُ قَوْلَ الَّتِي تُجَادِلُكَ فِي زَوْجِهَا وَتَشْتَكِي إِلَى اللَّـهِ وَاللَّـهُ يَسْمَعُ تَحَاوُرَكُمَا ۚ إِنَّ اللَّـهَ سَمِيعٌ بَصِيرٌ﴿١﴾الَّذِينَ يُظَاهِرُونَ مِنكُم مِّن نِّسَائِهِم مَّا هُنَّ أُمَّهَاتِهِمْ ۖ إِنْ أُمَّهَاتُهُمْ إِلَّا اللَّائِي وَلَدْنَهُمْ ۚ وَإِنَّهُمْ لَيَقُولُونَ مُنكَرًا مِّنَ الْقَوْلِ وَزُورًا ۚ وَإِنَّ اللَّـهَ لَعَفُوٌّ غَفُورٌ﴿٢﴾وَالَّذِينَ يُظَاهِرُونَ مِن نِّسَائِهِمْ ثُمَّ يَعُودُونَ لِمَا قَالُوا فَتَحْرِيرُ رَقَبَةٍ مِّن قَبْلِ أَن يَتَمَاسَّا ۚ ذَٰلِكُمْ تُوعَظُونَ بِهِ ۚ وَاللَّـهُ بِمَا تَعْمَلُونَ خَبِيرٌ﴿٣﴾فَمَن لَّمْ يَجِدْ فَصِيَامُ شَهْرَيْنِ مُتَتَابِعَيْنِ مِن قَبْلِ أَن يَتَمَاسَّا ۖ فَمَن لَّمْ يَسْتَطِعْ فَإِطْعَامُ سِتِّينَ مِسْكِينًا ۚ ذَٰلِكَ لِتُؤْمِنُوا بِاللَّـهِ وَرَسُولِهِ ۚ وَتِلْكَ حُدُودُ اللَّـهِ ۗ وَلِلْكَافِرِينَ عَذَابٌ أَلِيمٌ﴿٤﴾

Allaah Amekwishasikia kauli ya yule mwanamke anayejadiliana nawe (ee Muhammad صلى الله عليه وآله وسلم) kuhusu mumewe, na anamshitakia Allaah; na Allaah Anayasikia majibizano yenu. Hakika Allaah ni Mwenye kusikia yote, Mwenye kuona yote. Wale miongoni mwenu wanaowatamkia wake zao dhwihaar: Nyinyi kwetu kama migongo ya mama zetu.  Hao wake zao si mama zao. Hawakuwa mama zao isipokuwa wale waliowazaa. Na hakika wao bila shaka wanasema yasiyokubalika na kauli ya kuchukiza na uongo. Na hakika Allaah bila shaka ni Mwingi wa kusamehe, Mwingi wa kughufuria. Na wale wanaowatamkia wake zao dhwihaar, kisha wakarudi katika waliyoyasema (kuitengua dhwihaar), basi ni kuacha huru mtumwa kabla ya kugusana. Hayo mnawaidhiwa kwayo. Na Allaah kwa yale myatendayo ni Mwenye upeo wa khabari za dhahiri na za kufichika. Na yule asiyepata uwezo, basi afunge Swiyaam miezi miwili mfululuzo kabla ya kugusana. Na yule asiyeweza, basi alishe chakula masikini sitini. Hivyo ili mumuamini Allaah na Rasuli Wake. Na hiyo ni mipaka ya Allaah. Na makafiri watapata adhabu iumizayo. [Al-Mujaadalah :1-4]

 

 

Na Allaah Anajua Zaidi

 

 

 

 


Share