Nabiy 'Iysaa (عَلَيْهِ السَّلام) Ametabiriwa Katika Qur-aan Kuja Kwa Nabiy Muhammad (صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّم)?

 

Nabiy 'Iysaa (عَلَيْهِ السَّلام) Ametabiriwa Katika Qur-aan

Kuja Kwa Nabiy Muhammad (صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّم)?

 

Alhidaaya.com

 

SWALI:

 

Mimi naitwa *********** wa mbweni Zanzibar napenda kuuliza swali langu kwamba hivi kuna ukweli wowote kwamba yesu (Nabiy 'Iysa) alibashiria (alitabiri) juu ya ujaji wa Nabiy Muhammad s.w.a kupitia Biblia na Quran na kama upo naomba mnifafanulie.

 

 

JIBU:

 

AlhamduliLLaah - Himidi Anastahiki Allaah (Subhaanahu wa Ta’aala) Rabb wa walimwengu, Swalaah na Salaam zimshukie Nabiy Muhammad (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) na Swahaba zake (Radhwiya Allaahu 'anhum) na waliowafuata kwa wema mpaka Siku ya Mwisho

 

Kwanza kabla hatujajibu swali lako, tunakukumbusha kuwa unapoandika jina la Allaah au Nabiy usifupishe mbele yake kwa kuweka (S.W.) au (S.A.W.) kama ilivyozoelekea na wengi, bali andika kwa kirefu maneno hayo bila ya kuyafupisha. Andika (Subhaanahu wa Ta'aalaa) baada ya kumtaja Allaah, na andika Swalla Allaahu 'alayhi wa sallam) au (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) baada ya kumtaja Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam). Hivyo ndivyo inavyopaswa, na ndio heshima zaidi na utukufu na ndivyo inavyotamkwa na si kama inavyofupishwa na wengi kimazoea au kivivu. Pia hiyo ni ibada, na ibada inatakiwa ifanywe kwa namna iliyofundishwa na haifai kugeuza, kuongeza au kupunguza. Hali kadhalika

Swahaba walikuwa wakiandikiana barua na hakuna aliyekuwa akikatisha Salaam, wala kumswalia Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) wala kumtukuza Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) kwenye barua zao. Tuige na tufuate nyendo zao tusalimike.

 

Tufahamu kuwa utabiri huu hautoki kwa Nabiy 'Iysa (‘alayhis-salaam) bali ni wahyi kutoka kwa Allaah Aliyetukuka. Hilo si la ajabu kwani Rusuli waliokuja baada ya wengine walitabiri ujio wao. Ama Qur-aan iko wazi kabisa kuhusu hilo na Biblia nayo mbali ya kuwa ni mchanganyiko wa vitabu vingi lakini baadhi ya maneno ya Allaah Aliyetukuka yamebaki.

 

Ama Qur-aan inatuambia:

 

وَإِذْ قَالَ عِيسَى ابْنُ مَرْيَمَ يَا بَنِي إِسْرَائِيلَ إِنِّي رَسُولُ اللَّـهِ إِلَيْكُم مُّصَدِّقًا لِّمَا بَيْنَ يَدَيَّ مِنَ التَّوْرَاةِ وَمُبَشِّرًا بِرَسُولٍ يَأْتِي مِن بَعْدِي اسْمُهُ أَحْمَدُ ۖ فَلَمَّا جَاءَهُم بِالْبَيِّنَاتِ قَالُوا هَـٰذَا سِحْرٌ مُّبِينٌ﴿٦﴾

Na pale ‘Iysaa mwana wa Maryam aliposema: Enyi wana wa Israaiyl! Hakika mimi ni Rasuli wa Allaah kwenu mwenye kusadikisha yaliyo kabla yangu katika Tawraat na mwenye kubashiria kuja kwa Rasuli baada yangu jina lake: Ahmad. Basi alipowajia kwa hoja bayana, walisema: Hii ni sihiri bayana. [Asw-Swaff: 6]. Ahmad ni jina jingine la Nabiy Muhammad (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) kama iliyokuja katika Hadiyth sahihi.

 

 

Ama mabaki ya Biblia kuna utabiri mwingi wa hilo. Hilo ni lazima liwe hivyo kwani Allaah Aliyetukuka Anatuambia:

 

الَّذِينَ يَتَّبِعُونَ الرَّسُولَ النَّبِيَّ الْأُمِّيَّ الَّذِي يَجِدُونَهُ مَكْتُوبًا عِندَهُمْ فِي التَّوْرَاةِ وَالْإِنجِيلِ 

Wale wanomfuata Rasuli; Nabiy asiyejua kusoma wala kuandika ambaye wanamkuta ameandikwa kwao katika Tawraat na Injiyl, [Al-A'raaf: 157]. Hakika ni kuwa si Nabii 'Iysa tu aliyetabiri ujio wake bali Mitume wengine wengi. Hebu tutizame vifungu vifuatavyo:

  

  1. "Mtawala wa ulimwengu huu anakuja" (Yohana 14: 30).

 

  1. "Msaidizi, Roho Mtakatifu, ambaye Baba atamtuma kwa jina langu atawafundisheni kila kitu na kukumbusheni yote niliyokuambieni" (Yohana 14: 26).

  

  1. "Yeye ni roho wa ukweli" (Yohana 14: 16).

 

  1. "Afadhali mimi niende zangu, maana nisipokwenda Msaidizi hatakuja kwenu" (Yohana 16: 7).

  

  1. "Atakapokuja atawathibitishia walimwengu kwamba wamekosea kuhusu dhambi, uadilifu na hukumu ya Mungu" (Yohana 16: 8).

 

  1. Atawaongozeni katika ukweli (Yohana 16: 12 – 13).

  

  1. Ufalme wa Mungu utachukuliwa kutoka kwa Mayahudi na kupatiwa taifa litakalozaa matunda (Mathayo 21: 43).

 

 

Na Allaah Anajua zaidi

 

 

 

 

 

Share