Mashairi: Ya Habibi Ya Nabiya

 

Yaa Habibi Yaa Nabiya

 

Muhammad Faraj Salim As-Sa’ay (Rahimahu Allaah)

 

 

 

Maka ulikozaliwa, Madina ukapokewa

Kwa mashada ya mauwa, Yaa Habibi ya Nabiya

 

 

Maka ilikochomoza, Nuru ya Mola Muweza

Madina ikaangaza  kisha kote kueneya

 

 

Ulikuja na Risala, kutoka Kwake Ta’alaa
isomwe kila mahala, kila pembe ya duniya

 

Ni Risala kamilifu, Yake Mola Mtukufu
aso mwana wala kufu, yenye kunawiri njiya

 

 

Yote ukayatimiza, hapana ulichosaza
tena bila kupunguza, kamili kutufikiya

 

 

Ukatufunza Shahada,akhlaqi na ibaada
na kutoa misaada, kwa wenye kuhitajiya

 

Allahu katakasika, Mola Aso mshirika
ni Shahada ya hakika, na wewe wake Nabiya
 

 
Hiyo ndiyo ya awali, alotufunza Rasuli
ni nguzo iliyo ghali, nyoyoni mwetu jamiya

 

 
Swala akatufundisha, Asubuhi hadi Isha
zote twazikamilisha, nyakati zikiingiya

 

Twaziswali kwa wakati, kwa ikhilasi na dhati
tena bila hatihati, Ya Rabbi takabaliya

 

Kisha tutowe na Zaka, wakati unapofika
kwa hesabu kila mwaka, nisabu ikitimiya

 

Ilitiliwa mkazo, tajiri na walo nazo
tugawe bila vikwazo, tuwape wahitajiya

 

Kisha kutoa sadaka, hiyo kama tukitaka
mali inatakasika, na kurudisha afiya

 

Kuhiji Maka ni nguzo, kwa kila mwenye uwezo
hiyo haina mchezo, yataka kuipaniya

 

Kaaba nyumba tukufu, nyumba kongwe takatifu
hapo lazima utufu, shoti saba kutimiya

 

Nyumba hiyo ipo Maka, ni mji wenye baraka
Dhambi hapo hufutika, Mola Ametuambiya

 

 

Arafati ndiyo Hija,   huko nako kwakungoja
kwake aliye Mmoja, dua zinaelekeya

 

 

Siku hiyo ikifika,  watu tena patashika
machozi yamiminika, wakiomba na kuliya

 

Labeka Rabi labeka,  Mola Uso mshirika
Arafati tumefika,  Nawe watushuhudiya

 

 

Mwenye Sifa ya Uluwa, La ilaaha illa Huwa
ziwe zitakavyokuwa,  dhambi utatufutiya

 

 

Uturudishe tukiwa,  kama tulivyozaliwa

ndivyo tulivyoambiwa, na Muhammadi Nabiya

 

Kisha Mina siku tatu, wanakusanyika watu
wanapiga Jamaratu,  na kuchinja Adhuhiya

 

Yabaki shughuli moja, hiyo pia yakungoja
ni shoti saba za Hija,    Tawafu na Sayi piya

 

 

Safari ikishafika,  ukataka kuondoka

usibaki hapo Maka Widaa itabakiya

 

 

Hiyo ni tawafu moja, ukesha moja kwa moja

Hapana tena kungoja Garini utaingiya

 

Hizo ndizo nguzo zake, na hiyo Risala yake
kutoka kwa Mola wake, ni amana ya Jaliya

 

Ni nzito kweli kweli, Ilikataa jabali
wewe ukaikubali, kubeba ukairidhiya

Mola Amekuhitari,  mbele ya wote bashari
uifikishe habari, kwa jini na insiya

 

 

Anachokitaka huwa, Mwenyewe kakuchaguwa
kwa sababu akujuwa,  kipenzi chake Nabiya

 

Mwenye khuluqa adhimu, mpole tena karimu
kwa uma wake rahimu, kuliko kila Nabiya

 

 

Ni mwenendo mtukufu, ulotimu kamilifu
mkweli muaminifu mwenye sifa maridhiya

 

Mfano wa Quruani,  inotembea njiani
kakufundisha Manani, utukufu wa tabiya

 

 

 

 

 

 

Share