Imaam Ibn Baaz: Tahiyyatul-Masjid Inaweza Kuswaliwa Katika Nyakati Zilizokatazwa?

Tahiyyatul-Masjid Inaweza Kuswaliwa Katika Nyakati Zilizokatazwa?

 

Imaam Ibn Baaz (Rahimahu Allaah)

 

www.alhidaaya.com

 

 

SWALI:

 

Kuna mazungumzo mengi kuhusiana na Tahiyyatul Masjid. Kuna wanaosema haipaswi kutekelezwa nyakati zilizokatazwa kuswaliwa Swalaah, kama zile nyakati za kuchomoza jua, na kuzama jua.

Wengine husema inaruhusiwa maadam sababu ya kuswaliwa Swalaah hiyo, haijawekewa vikwazo vya nyakati zozote, na inapaswa kuswaliwa hata kama nusu ya jua litakuwa limeshazama.

Naomba ufafanuzi wa kina kwa suala hili.

 

 

JIBU:

 

Kuna Ikhtilaaf baina ya Wanachuoni kuhusu suala hili, lakini mtazamo sahihi ni kuwa, Tahiyyatul-Masjid ni rukhsa kuswaliwa katika nyakati zote, hata kama ni baada ya Al-Fajr au hata baada ya Al-‘Aswr kutegemea maana ya maneno ya jumla ya Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam):

 

“Atakapoingia yeyote katika nyinyi Msikitini, hapaswi kukaa hadi aswali rakaa mbili.” [Al-Bukhaariy na Muslim]

 

Vilevile, hiyo ni Swalaah ambayo ina sababu ya kuitekeleza kama vile Swalaah ya kutufu ‘Swalaatut-Twawaaf’ (Rakaa mbili zinazoswaliwa kufuatia kuzunguka Al-Ka’bah katika kipindi cha Hajj na ‘Umrah), na ‘Swalaatul-Kusuwf’ (Swalaah ya kupatwa kwa jua au mwezi), na rai iliyo sahihi ni kuwa, Swalaah zote hizi huweza kuswaliwa nyakati zozote zile zinapohitajika kuswaliwa hata kama ni katika zile nyakati ambazo zimekatazwa kuswaliwa Swalaah, kama vile ambavyo huswaliwa zile Swalaah za Fardhi za kulipwa ambazo mtu amezikosa, kwa mujibu wa maneno ya Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) kuhusiana na Swalaah ya Twawaaf:

 

“Enyi watu (wa kabila la) ‘Abdi Manaaf! Msimzuie yeyote kufanya Twawaaf katika Nyumba hii, na kuswali nyakati zozote zile za usiku au mchana anapotaka.” [Abuu Daawuwd, At-Tirmidhiy, Ahmad]

 

Na amesema (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) kuhusiana na Swalaah ya kupatwa kwa jua au mwezi:

“Hakika jua na mwezi ni alama mbili miongoni mwa alama za Allaah, hazipatwi kwa kifo au kuzaliwa mtu yeyote, hivyo, pindi unapoona hizo (zikipatwa), swali na uombe du’aa, hadi linapokusibu liondoke.” [Al-Bukhaariy na Muslim]

 

Na kadhaalika, amesema (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam):

“Yeyote anayelala akapitwa na Swalaah au akasahau, basi alipe pindi tu atakapokumbuka, na hakuna kafara isipokuwa hiyo.” [Al-Bukhaariy na Muslim]

 

Hadiyth zote hizi, zinaonesha kujumuishwa nyakati ambazo Swalaah zimekatazwa kuswaliwa na nyakati nyinginezo.

 

Maelezo haya, yamefadhilishwa na Shaykh Al-Islaam Ibn Taymiyyah na mwanafunzi, Mwanachuoni mkubwa, Ibn Al-Qayyim (Rahimahumu Allaah).

 

Na Allaah ni mwenye kutoa Tawfiyq.

 

 

[Imaam ‘Abdul-‘Aziyz Ibn Baaz, Fataawa Al-Islaamiyyah, juz. 2, uk. 286]

 

Share