Mwanamke Mchawi Anatekeleza Sana Ibada Lakini Anafanya Uchawi Wa Kuua Watu, Vipi Ibada Zake?

 

Mwanamke Mchawi Anatekeleza Sana Ibada Lakini

Anafanya Uchawi Wa Kuua Watu, Vipi Ibada Zake?

 

Alhidaaya.com

 

 

SWALI:

 

Kuna mwanamke mmoja hapa Oman ameshika dini sana suna zote anafunga,salaa zote anasali and mara kwa mara anafungu Miezi Miwili Mfululizo (Siku) 60 Tawbat Nasuha "Shahareen Mutatabien" Lakini ni mchawi mkubwa sana hata watu wengi wamemshika uchawi.

 

Siku moja tulimuuliza mtoto wake wa kiume ambaye ameshika dini sana" nini jazaa ya mtu mchawi anatoa watu na anaweka watu vitandani ikiwa yeye ni mcha Allaah bila ya kumtaja mama yake, Jibu Lake Kuwa Kama Mtu Chawi anafanya ibada zote zinazotakiwa na anakwenda hajj, anafunga tawbat nasuha basi Allaah Anamfutia Dhambi Yake Yote Aliyoyafanya. Je ni kweli maana nasikia mtu mtu aliyemuua mwenzake hana msamah mbele ya "Allaah"

 

JIBU:

 

Sifa zote njema Anastahiki Allaah Aliyetukuka Rabb Mlezi wa walimwengu wote, Swaalah na salamu zimshukie kipenzi chetu Nabiy Muhammad (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) na Swahaba zake (Radhwiya Allaahu 'anhum) na watangu wema mpaka Siku ya Mwisho.

 

Kushika dini kwa mtu kunajulikana na kueleweka kutokana na kushikamana huyo muhusika na kila alilokuwa ameshikamana nalo au amefundisha na kulishauri Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) na sio kushikanama na matamanio ya nafsi yake; Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) ndiye tunayeweza kusema pekee ameshika dini sana na juu ya kushika kwake dini yeye (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) anamjua Allaah na kumcha kuliko sisi sote na hata hivyo kama ilivyothibiti hakuwa kufunga miezi miwili mfululizo. Qur-aan imewataka kufunga miezi miwili watu kwa makosa maalumu na sio kujifungia tu, wenye kufunga miezi miwili kwa mfululizo huwa ima ameua Muislamu kwa bahati mbaya (si kwa makusudi) kama inavyosema Qur-aan: 

وَمَا كَانَ لِمُؤْمِنٍ أَن يَقْتُلَ مُؤْمِنًا إِلَّا خَطَأً ۚ وَمَن قَتَلَ مُؤْمِنًا خَطَأً فَتَحْرِيرُ رَقَبَةٍ مُّؤْمِنَةٍ وَدِيَةٌ مُّسَلَّمَةٌ إِلَىٰ أَهْلِهِ إِلَّا أَن يَصَّدَّقُوا ۚ فَإِن كَانَ مِن قَوْمٍ عَدُوٍّ لَّكُمْ وَهُوَ مُؤْمِنٌ فَتَحْرِيرُ رَقَبَةٍ مُّؤْمِنَةٍ ۖ وَإِن كَانَ مِن قَوْمٍ بَيْنَكُمْ وَبَيْنَهُم مِّيثَاقٌ فَدِيَةٌ مُّسَلَّمَةٌ إِلَىٰ أَهْلِهِ وَتَحْرِيرُ رَقَبَةٍ مُّؤْمِنَةٍ ۖ فَمَن لَّمْ يَجِدْ فَصِيَامُ شَهْرَيْنِ مُتَتَابِعَيْنِ تَوْبَةً مِّنَ اللَّـهِ ۗ وَكَانَ اللَّـهُ عَلِيمًا حَكِيمًا ﴿٩٢﴾

Na haiwi kwa Muumin amuue Muumin ila kwa kukosea tu. Na atakayemuua Muumin kwa kukosea basi aachilie huru mtumwa Muumin na atoe diya kwa kuifikisha kwa ahli zake, isipokuwa watolee wenyewe swadaqah. Na ikiwa ni miongoni mwa watu wa maadui zenu naye ni Muumin, basi (aliyeua) aachilie huru mtumwa Muumin. Na ikiwa ni miongoni mwa watu ambao kuna mkataba baina yenu na baina yao; basi wapewe diya kuifikisha kwa ahli wake na aachiliwe huru mtumwa Muumin. Asiyepata, afunge Swiyaam miezi miwili mfululizo; kuwa ni tawbah kwa Allaah. Na Allaah daima ni Mjuzi wa yote, Mwenye hikmah wa yote.  [An-Nisaa: 92]

 

Au amemuingilia mkewe mchana wa Ramadhwaan, au amejitenga na mkewe kwa kufanya dhwihaar.

 

Kusema kuwa ameshikamana na dini na halafu ukasema kuwa Lakini ni mchawi mkubwa sana ni mambo mawili yenye kwenda upande mmoja bila ya kuweza kukutana au kushikana mpaka mwisho wa huu ulimwengu; kwani uchawi ni moja katika mambo yenye kupingana na kwenda kunyume na itikadi ya Kiislamu; na ni jambo lenye kuuvunja Uislamu wa mtu na ni katika madhambi makubwa 'Al-Kabaair' na ni miongoni mwa mambo saba yenye kuhilikisha 'Muwbiqaat' kwani mchawi ni lazima awe amekufuru kama inavyothibitisha Qur-aan:

وَلَـٰكِنَّ الشَّيَاطِينَ كَفَرُوا يُعَلِّمُونَ النَّاسَ السِّحْرَ وَمَا أُنزِلَ عَلَى الْمَلَكَيْنِ بِبَابِلَ هَارُوتَ وَمَارُوتَ ۚ وَمَا يُعَلِّمَانِ مِنْ أَحَدٍ حَتَّىٰ يَقُولَا إِنَّمَا نَحْنُ فِتْنَةٌ فَلَا تَكْفُرْ ۖ

"lakini mashaytwaan ndio waliokufuru; wanafundisha watu sihiri na yaliyoteremshwa kwa Malaika wawili katika (mji wa) Baabil; Haaruwt na Maaruwt. Nao wawili hawamfundishi yeyote mpaka waseme: Hakika sisi ni mtihani, basi usikufuru" [Al-Baqarah: 102].  

 

Ndugu yetu huyo, inapasa afahamishwe kuwa uchawi ni katika ‘amali ya Shaytwaan na ni haraam kwani inamvua Uislamu wake. Uchawi haupatikani isipokuwa kwa kupitia mambo yenye ushirikina na kujidai kujua mambo ya ghayb na yote yanakwenda kinyume na Uislamu na mafundisho ya Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam). Mpeni nasaha arudi kwa mola wake na atubie kwani, mchawi pamoja ya kuwa ni mshirikina, bado anaweza kutubia na tawbah yake ni kuacha uchawi mara moja na kujuta na kurudi kwa Rabb wake na kutorejera tena mpaka ‘amali za uchawi na kila lenye kufungamana na uchawi mpaka akutane na Rabb wake, na huenda tawbah yake ikakubaliwa akiwa mkweli.

 

Pia nasaha zetu kwako na kwa kila Muislamu tuwe tunashikamana na mafundisho ya dini na miongoni mwa mafundisho ni kuwa tusiwe mafasiki kwa kuzua jambo bila ya uhakika. Wala tusiwe ni wenye kudadisi mambo kama haya au kuwasingizia watu au kuwasema watu huenda tukawa tunaingia katika moja kati ya Aayah mbili za Al-Hujuraat; Qur-aan inasema: 

يَا أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُوا إِن جَاءَكُمْ فَاسِقٌ بِنَبَإٍ فَتَبَيَّنُوا أَن تُصِيبُوا قَوْمًا بِجَهَالَةٍ فَتُصْبِحُوا عَلَىٰ مَا فَعَلْتُمْ نَادِمِينَ﴿٦﴾

Enyi walioamini! Anapokujieni fasiki kwa habari yoyote, basi pelelezeni, msije mkawasibu watu kwa ujahili, mkawa kuwa wenye kujuta juu ya ambayo mmeyafanya." [Al-Hujuraat: 6]

au,

يَا أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُوا اجْتَنِبُوا كَثِيرًا مِّنَ الظَّنِّ إِنَّ بَعْضَ الظَّنِّ إِثْمٌ ۖ وَلَا تَجَسَّسُوا وَلَا يَغْتَب بَّعْضُكُم بَعْضًا ۚ أَيُحِبُّ أَحَدُكُمْ أَن يَأْكُلَ لَحْمَ أَخِيهِ مَيْتًا فَكَرِهْتُمُوهُ ۚ وَاتَّقُوا اللَّـهَ ۚ إِنَّ اللَّـهَ تَوَّابٌ رَّحِيمٌ﴿١٢﴾

Enyi walioamini!  Jieupusheni sana na dhana kwani hakika baadhi ya dhana ni dhambi. Na wala msifanyiane ujasusi, na wala wasisengenyane baadhi yenu wengineo. Je, anapenda mmoja wenu kwamba ale nyama ya nduguye aliyekufa? Basi mmelichukia hilo! Na mcheni Allaah! Hakika Allaah ni Mwingi wa kupokea tawbah, Mwenye kurehemu. [Al-Hujuraat: 12]

 

Ama kuhusu maelezo yako kuwa mtu aliyemuua mwenzake hana msamaha mbele ya Allaah haya ni katika habari ambazo si sahihi, na kama ameua kama unavyodai basi ni katika madhambi makubwa 'Al-Kabaair na kila muuaji ana hukumu yake kulingana na namna ya mauaji yake na hakuna kosa katika Uislam lisilokuwa na tawbah.

 

 

Na Allaah Anajua zaidi

 

 

 

Share